MUNGU WETU NI MOTO ULAO WAEBRANIA 12:29.

Wednesday, February 16, 2011

JE ALIYEKUKOSEA ASIPOKUOMBA MSAMAHA UFANYEJE?





"Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwana neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu.Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu" (Marko 11:25,26)



Yesu Kristo aliyasema maneno haya kwa wanafunzi wake wa kwanza, alipokuwa akiwafundisha juu ya imani. Maneno haya ya Yesu Kristo, yanatuhusu hata sisi tulio wanafunzi wake siku hizi.Yesu Kristo katika maneno haya anazungumza na mwanafunzi wake aliyekosewa na mtu mwingine.Na katika somo hili, toka mwanzo tumechukua mtazamo huu wa Yesu Kristo; tunazungumza na mtu aliyekosewa na mtu mwingine.Somo hili lina maneno yenye mafundisho kwa mtu ambaye amekwazwa na mwenzake;mtu aliyefanyiwa kosa lolote lile.Kuna watu wengi sana wanaokosewa na watu wengine. Na tunaamini hata wewe kuna wakati fulani katika maisha yako umekwazwa na mtu mwingine.Katika ndoa makwazo yamekuwa kitu cha kawaida. Maofisini watu wanakosana kila siku. Hata na katikati ya watu wa Mungu, makwazo yanatokea mara kwa mara.Na sehemu mojawapo muhimu katika maisha ya mkristo ni maombi. Na ili tuwe na maisha ya maombi yenye mafanikio, ni lazima tuwe watu wenye tabia ya kusamehe waliotukosea.Yesu Kristo alijua jambo hili na umuhimu wa kusamehe KWANZA kabla ya kuanza kuomba.Yesu Kristo alisema, " Ninyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu".Maneno haya hayatupi uchaguzi wa kusamehe mtu wakati tunapopenda tu au wakati tunapotaka.Maneno haya ni agizo la Bwana Yesu Kristo ambalo linatakiwa lifuatwe na kila mwanafunzi wake, ili aweze kuwa na mafanikio katika maombi yake.



Unatakiwa kusamehe mara ngapi?



Mama mmoja ambaye alikuwa ana matatizo katika unyumba wake, alisikika akisema maneno haya:"Mume wangu amenitesa kwa muda mrefu sasa; na hali ya mambo ilivyo, sidhani kama naweza hata kumsamehe tena; maana nimemsamehe nimechoka".Ni kweli kabisa kwamba mtu mwingine anaweza kukukosea mara nyingi sana. Hii huwa mara nyingi inatokea kwa watu ambao wanakaa pamoja au ni majirani.Hali ya mama huyu aliyesema maneno hayo, inawapata watu wengi sana, na nina uhakika watu hao wamechoka na hali hiyo.



Inawezekana wewe ni mke wa mume ambaye ni mlevi, malaya, na mgomvi. Kila akirudi nyumbani ni kukutukana na hata wakati mwingine kukupiga. Na umeomba kwa Mungu juu ya jambo hili kwa muda mrefu bila kuona mafanikio.Sasa umeamua ufanyaje wakati unaona unazidi kuonewa na kuteswa? Inawezekana wewe ni mume wa mke ambaye ni mlevi, malaya na mgomvi. Inawezekana wewe ni mzazi wa watoto ambao hawakusikii, walevi, malaya, na wahuni.Inawezekana wewe ni mfanyakazi katika ofisi ambayo unaonewa haki zako za kupanda cheo, kupanda mshahara na marupurupu mengine, bila sababu yoyote.Sasa, nakuuliza, umeamua kuwachukulia hatua gani hao watu waliokukosea?Kumbuka wewe ni mkristo, na unatakiwa uamue mambo yako kikristo, kwa kulifuata Neno la Mungu.Hawa watu wanaotukosea tunatakiwa kuwasamehe mara ngapi? Hili swali ni muhimu, kwa kuwa watu wengine hawachoki kuwakwaza wengine!



Imeandikwa:"Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye;akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba,akisema, Nimetubu, msamehe" (Luka 17:3,4):



Ni kweli kabisa! Mtu akikukosea na akitubu ni rahisi kumsamehe. Lakini ikiwa mtu aliyekukosea asipokuja kutubu je naye anahitaji kusamehewa?Hata asipotubu msamehe.Hili ni jambo ambalo inabidi tulizungumze kwa kufuata Neno la Mungu; maana ni jambo linalowasumbua wengi.Kuna wakati fulani tulikuwa tunalijadili jambo la kusamehe na wenzetu. Mmoja kati ya wale waliokuwepo alisema hivi: "Mimi siwezi kumsamehe mtu aliyenikosea asipokuja kutubu".Inawezekana hata wewe una mawazo kama haya. Lakini nakuuliza swali hili, "Je, kuna mstari wo wote katika biblia unaosema mtu aliyekukosea asipotubu usimsamehe?".



Sisi hatujawahi kuuona. Kama upo tunaomba utuambie.Huhitaji kuombwa msamaha ili upate kusamehe. Biblia inasema; ‘Utusamehe deni zetu, kama sisi tuwasamehevyo wadeni wetu’ Biblia haikusema ‘Utusamehe deni zetu, kama sisi tuwasamehevyo waliotuomba msamaha!Kwa hiyo tunatakiwa kuwasamehe waliotukosea hata kama hawakutuomba masamaha.Hii ni kweli. Na sasa tuone neno la Mungu linatuambia nini:



"Kisha Petro akamwendea akamwambia, Bwana,ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? Yesu akamwambia, si kuambii hata mara saba,bali hata saba mara sabini" (Mathayo 18:21,22)



Hapa hatuoni Yesu Kristo akimwambia Petro kuwa mtu ni lazima atubu ili asamehewe. Ila anamjibu kuwa "Sikuambii hata mara saba, bali saba mara sabini"Petro alifahamu ya kuwa anahitaji kusamehe hata asipoombwa msamaha. Tatizo lake lilikuwa ni asamehe mara ngapi.Kumbuka ya kuwa unayaweza mambo yote, pamoja na kusamehe bila kuombwa msamaha, katika yeye akutiaye nguvu (Wafilipi 4:13) Tena kumbuka ya kuwa ni tabia ya Mungu iliyo ndani yako (2Petro 1:3,4) inayokuwezesha kusamehe na kusahau hata kama hujaombwa msamaha.Kumbuka si wewe unayekosewa na kukwazwa, bali Kristo aliye ndani yako. Kwa kuwa ulipompokea Kristo katika moyo wako, ulifanyika kuwa kiumbe kipya. Si wewe unayeishi, bali Kristo ndani yako (Wagalatia 2:20)



MUNGU ALITUSAMEHE KABLA SISI HATUJAMUOMBA MSAMAHA WALA KUTAMBUA KOSA LETU.MUNGU ALITULIPIA DENI LETU LA DHAMBI KABLA SISI HATUJAMUOMBA MSAMAHA.



Kwa maana imeandikwa: "Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi" (Warumi 5:8)."…….Kristo alikufa kwa ajili yetu tulipokuwa tungali wenye dhambi". Maana yake tulipokuwa bado hatujaomba msamaha Yesu alikufa kwa ajili yetu. Mshahara wa dhambi ni mauti (Warumi 6:23). Na kwa kufa Kristo inamaanisha tumesamehewa na kulipiwa deni letu. Kazi tunayotakiwa kuifanya ni kuupokea msamaha kwa njia ya toba.



Hata Yesu Kristo alipoteswa na kusulubiwa, na kufa msalabani, aliwasamehe waliomsulubisha na akawaombea msamaha (Luka 23:34); KABLA ya kuombwa msamaha.Na ni sauti ya Yesu Kristo inayosema ndani yako ukikosewa na mtu; "Msamehe kwa kuwa hajui alitendalo". Na Yesu akisema msamehe mtu, basi huna budi kusamehe.Na kumbuka unatakiwa kusamehe KWA AJILI YAKO MWENYEWE, hata kama hujaombwa msamaha ili na wewe

1 comment:

avold one said...

Kaka MUNGU na akubariki sana kwa maneno yako mazuri,inapendeza sana ikiwa tunamkumbuka yeye anayetuwezesha kupumua kila iitwapo leo. Big up.